Monday, July 27, 2015

HATA HAPO ULIPO TUMAINI-Na:- BRYSON LEMA (RP)


JUMAPILI:  26 JULY 2015 - UFUFUO NA UZIMA MOROGORO

 

Utangulizi: Katika maisha ya kila siku,tunapita katika vitu vigumu na vizito. Ulalapo usiku,  huwa unamshukuru Mungu kwa sababu siku kama ile maishani mwako haijirudii tena. Hata hivyo imeandikwa katika  2WAFALME 18:19 kwamba…[Yule amiri  akawaambia, Haya, mwambieni Hezekia, kusema, Mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru, asema hivi, Ni tumaini gani hili unalolitumainia?]… Hata sisi ndivyo ilivyo kwamba kuna nyakati tunajiona hatufai tena. Ujue kuwa tatizo lako halipo kwenye ile shida uliyo nayo, bali lipo kwenye ‘tumaini’ ulilo nalo maishani mwako. Jambo la kwanza ni kubadilisha mtizamo wako, bila kuhesabu idadi ya miaka yako kwenye wakovu. Yesu Kristo alipoambiwa na Shetani ageuze jiwe liwe mkate, alimjibu shetani kuwa “mwanadamu hataishi kwa mkate tu bali kwa kila neno litokalo kinywani mwa Mungu”.  Weka macho yako kwenye tumaini lako.



Tatizo ulilonalo ni dogo mno bali tatizo lipo kwenye tumaini unalolitumainia. Musa hakuona Bahari ya Shamu kama kikwazo chake, kwa sababu ile bahari haikuwa pale kwa ajili ya kumuangamiza. Wana wa Israeli waliotoka Misri walikuwa ni  wengi sana, lakini ni wawili  tu waliofika nchi ya Ahadi, (Joshua na Kaleb). Siyo kwamba watu hawa wawili hawakuwaona wale manefili,  lakini kilichowasaidia ni kuwa na tumaini kwa Mungu wa Israeli. Watu hawa wawili waliweza kwa sababu tumaini lao lilikuwa kwa Mungu. Tumaini lako umeliweka wapi? Je, unamwekea tumaini ndugu yako kwa sababu amesoma sana? Kumbuka kuwa, Mungu huyo huyo aliyewaokoa wana wa Israeli ndiye aliyewaangamiza pia wale Wamisri.

 

Tumaini ni kama usukani ndani ya mwanadamu. Hivyo bila tumaini huwezi kwenda. Wengi akili zetu zinakuwa zimetengeneza picha, inaweza ikawa "picha za kushindwa au kushinda". Maisha ya mwanadamu ni kama msafiri na dereva uliye naye ni tumaini ulilonalo je litakufikisha salama. Unapokuwa na tumaiani ndani ya Yesu Kristo haijalishi tatizo ulilonalo. Angalia maisha yako ni kwanini hofu na mashaka zimejaa ndani yako? Ni kwa sababu umekosa tumaini katika maisha yako.Hata Yesu Kristo hakuwaponya wagonjwa wote.  Yesu alikuwa anaangalia tumaini la mtu lipo wapi. Shetani  hupenda sana kuchenzea akili za watu kwenye eneo la tumaini.  

 

Imeandikwa katika ISAYA 12:2…[Tazama, Mungu ndiye wokovu wangu;  Nitatumaini wala sitaogopa;  Maana Bwana YEHOVA ni nguvu zangu na wimbo wangu;  Naye amekuwa wokovu wangu.]… Isaya anasema Mungu ndiye tumaini lake naye hataogopa. Anasema hivi kwa sababu hofu ndio kitu cha kwanza kinachoondoe “tumaini”. Siri kubwa ya shetani ni kukuingiza hofu,  ili zipeperushe kila tumiani la watu kwa Mungu. Ili kushinda tatizo siyo  kulikimbia tatizo, bali ni kupita katikati ya hilo tatizo. Vita vikiinuka kazini, suluhisho siyo kukimbia hiyo kazi, bali mtafute aliyesababisha tatizo  na kushughulika na ile roho ya hilo tatizo ndani mwake.  Kulikimbia tatizo siyo ushindi dhidi ya hilo tatizo, bali ni sawa na kuahirisha hilo tatizo. Mungu tunayemtumikia sisi anataka tupambane na adui zetu na siyo kuwakimbia. Unapotaka kuitwa mpiganaji, lazima upigane. Ili uitwe shujaa ni lazima upambane.

 

Mtu yule anayepigwa ngumi ndiye anayejua uzito wa ngumi.Tunaona wana wa Israeli walipo uzunguka ukuta wa Yeriko bila wao kujua kila siku walipozunguka walikuwa wanarusha ngumi, na siku ya saba ilipofika ukuta ukaanguka. Na ulipoanguka Yoshua akasema na alaaniwe atakaye jenga tena huu ukuta. Kumbe ukuta unapoanguka laana hutolewa palepale. Hivyo hata wewe rusha ngumi juu ya adui zako. Kila unaporusha ngumi misuli yako inabadilika na inakuwa si ya kawaida, ni kama Samson alivyowekwa gerezani na kuanza kusaga ngano, Kila siku alipokuwa akisaga ngano kulimpa nguvu na uwezo misuli kukua. Tunaona siku aliyoangusha nguzo aliweza kuuwa watu wengi mno kuliko  kipindi cha nyuma.

 

Yesu Kristo aliliweka tumaini lake kwa Mungu, na ndiyo maana akiwa pale msalabani alimwambia Yule mwizi kuwa “Hakika, leo hii tutakuwa wote paradiso”. Imeandikwa katika YOHANA 14:1-3…[Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. 2 Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. 3 Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.]… Usiweke tumaini lako kwa mwanadamu, bali kwa Yesu Kristo, ambaye alisema anaenda mbinguni kuandaa makao,  ili alipo yeye na  wewe uwepo.   Ni Yesu pekee aliyesema alipo yeye anataka na wewe uwepo, hivyo ndio mtu unayetakiwa kumtumainia. Ukimtumainia Yesu atakupa unacho hitaji.

 

Kuna msemo unasema aliyeshiba hamwangalii mwenye njaa. Hivyo usitegemee kusaidiwa hata na ndugu yako maana anaweza asikusaidie. Acha kumtumainia mwanadamu maana inapotokea hatari atatafuta usalama wake kwanza na baada ya hapo ndipo ataangalia kama kuna nafasi kwa ajili yako ili akusaidie.

 

Siri ya mkristo wa kweli ni kupigana. Utaona Bwana asema, Bwana ni mtu wa vita, Bwana ndio jina lake. Pia anasema hiki ndio chuo cha vita. Hivyo kama mkristo ni lazima uingie kwenye chuo cha vita na upigane. Pale unapokuwa na shida ndipo mahali Mungu anajitokeza. Tunaona hata Musa alipokuwa kwa Farao penye raha, Mungu hakuweza kusema naye lakini tunaona Mungu aliweza kusema naye kwenye kichaka mahali ambapo hapakuonekana kama panafaa. Hivyo inatakiwa tatizo ulilonalo ng’ang’ania hapo hapo pambana na upigane. Hilo tatizo lililoko mbele yako ni la kupiga, haupaswi kuliogopa. Unapoiona dhahabu, ujue upo mwamba mgumu ulipasuliwa hadi ikapatikana. Unapoona mtu amefanikiwa ujue mtu huyo amepambana hadi amefanikiwa. Hivyo ili ufanikiwe ni lazima upambane.

 

Kuna vitu viwili kwa mwandamu miaka na hatma. imeandikwa katika YOHANA 17:1-4.. [Maneno hayo aliyasema Yesu; akainua macho yake kuelekea mbinguni, akasema, Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe; 2 kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. 3 Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma. 4 Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye.]… Tunaona Yesu anasema Baba kazi yako uliyonipa nimeimaliza. Ina maana alikamilisha ile hatma yake baada ya miaka ile kuisha. Tunaona wana wa Israeli walikaa utumwani miaka 430 badala ya 400 ili kwenda Kanaani, NCHI YA AHADI, kwa sababu hawakujua muda. Ila baada ya Mungu kusikia kilio chao ndipo alipowatoa utumwani. Hivyo nawe ni lazima umlilie Bwana ili asikie kilio chako.

 

Kazi kubwa ya shetani ni kukufanya uogope. ZABURI 20:7…[Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.]…. Ukilitaja jina la Bwana Mungu wa majeshi, utakuwa na ushindi katika safari ya maisha yako. Ukitaka kuwa mfalme kama alivyokuwa Daudi, usitaje magari wala farasi bali taja jina la Yesu.Daudi akasema toka ujana wake hadi uzee hajawahi kumuuona mwenye haki akitangatanga na kuomba barabarani. Hivyo tumaini lako liweke kwa Yesu maana hata kuacha uaibike.

 

Endapo Mtu hujaokoka, leo  ni fursa nyingine kwa  wewe kufanya maamuzi hayo,  ili uweze kupata ushindi sawasawa na ahadi za Mungu maishani mwako.

 

=== © Information Ministry ===

(Ufufuo Na Uzima - Morogoro)

Mtaa wa Nguvu Kazi, (Minara Mitatu), Mkundi-Morogoro.

 /or

Contact our Church Leadreship:

 Bishop Dr. Godson Issa Zacharia

 (Glory of Christ (Tanzania) Church inMorogoro)

Cellphone: (+255) 765979866 /or +255 713459545

 
Share:

Monday, July 20, 2015

SOMO: MGAWO WA KISHETANI-Na: BRYSON LEMA (RP)


JUMAPILI:  19 JULY 2015 - UFUFUO NA UZIMA MOROGORO

 
 
 

Utangulizi: Upo "mgawo wa kishetani" kwenye maisha ya wanadamu. Katika Kitabu cha MIKA 2:4 imeandikwa hivi:…[Siku hiyo watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na kusema,  Sisi tumeangamizwa kabisa;  Yeye analibadili fungu la watu wangu;  Jinsi anavyoniondolea hilo! Awagawia waasi mashamba yetu.]…. Jambo la muhimu  katika andiko  hili  ni kuwa kuna mgawo, tena wa mashamba. Na kama kuna mgawo, ujue yupo  mwenye kugawa. Swali la  kujiuliza hapa ni kuwa,  kwa nini mashamba haya yagawiwe kwa waasi? Maana yake, mali zangu,  vitu vyangu vimegawiwa kwa shetani, kwa sababu Biblia inamuonesha shetani kuwa aliasi kule mbinguni. Na kwa hiyo sasa, huyu  shetani amevikamata vitu vyangu,  akavifanya  kama vyake.

 

Ukisoma YEREMIA 1:5 imeandikwa:…[Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa.]… maana yake,  kabla ya Yeremia kuzaliwa,  alishagawiwa mgawo wake unaomhusu.  Alitakiwa  aende katika mafanikio yake kwa sababu tayari anao mgawo wake kutoka kwa muumba wake, yaani Mungu (Jehovah).

 

Shetani alichokifanya ni kutuibia.  Biblia inasema katika YOHANA 10:10 [Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.]. Ndani ya maisha yako,vipo vitu unavyopitia visivyo kuwa vya kwako. Maana yake,  una vitu ambavyo unaviona kama vyako lakini kumbe ni  mgawo wa kishetani”. Walipokaa mashetani na mawakala wao, walikutengenezea ugonjwa,  na ambao unakaa nao kwa muda mrefu sasa, na hata imefikia wakati umeanza kuuita huo ugonjwa kuwa ni ‘ugonjwa wangu’.  Ayubu  vivyo hivyo, alipata magonjwa na adha mbalimbali, lakini vyote hivi hakugawiwa na Bwana, bali ulikuwa mgawo wa kishetani. Kosa ambalo wengi wameendelea kulikiri leo hii ni kuungana na maneno ya Ayubu kusema ‘Bwana ametoa, na Bwana ametwaa”. Siyo kweli  kwamba Bwana anapokupa anakuja mara ya pili  kutwaa kile alichokupatia.  Ingekuwa hivyo basi Ibrahimu alipoambiwa amtoe sadaka mwanae pekee Isaka,  basi siku ile ile Isaka angechinjwa. Ili kudhihirisha hili, Bwana hakuruhusu Isaka afe, na badala yake alimuepusha na kifo kile cha kutolewa sadaka na Ibrahimu baba yake.

 

Upo mgawo wa kishetani unaong’ang’ania maisha yako. Wakati mwingine unajikuta kuna mambo unashindwa kuyaacha maishani mwako kwa sababu tayari huo ni mgawo. Imeandikwa EZEKIELI 23:7…[ Akawagawia mambo yake ya kikahaba, watu wateule wa Ashuru, wote pia; akajitia unajisi kwa vinyago vyote vya kila mmoja wa hao aliowapenda.]… Unapoupata mgawo, huo mgawo unakuwa sehemu ya maisha yako. Ndiyo maana unakuta maisha ya mtu yanakuwa magumu kwa sababu kuna mgawo wa kishetani ndani ya  maisha yake, na siku ya leo ni maalumu kwa ajili ya kumrudishia  shetani migawo yake kwa Jina la Yesu.

 

Mwanadamu mara  zote anakuwa na Tabia ya kukataa mambo mapya.  Hata hivyo, baada ya mambo mapya kuanza na kuyazoea, mwanadamu husahau kuwa mwanzoni  hakuwa anafurahia hali hiyo. Mfano ni pale ambapo mtoto wakati wa kuzaliwa, hulia kwa sababu alishazoea maisha ya kukaa kwenye tumbo la mama yake,  na hivyo kukaa duniani nje ya hilo tumbo  hataki. Hata hivyo, baada ya mtoto huyu  kuzaliwa na kuzoea dunia, hapendi tena kutoka humu duniani (kufa),  kwa sababu ameshazoea maisha ya kuwa humu duniani. Ndivyo ilivyo hata kwa baadhi ya watu wanapopata matatizo. Mwanzoni mtu huyakataa matatizo/magonjwa/ au mateso fulani, na huwa tayari kuyakemea, lakini  matatizo haya yakiendelea kukaa kwa miaka miwili  na kuendelea, mtu huyazoea matatizo hayo na kuyafanya kuwa sehemu ya maisha ya huyo mtu.

 

Yesu Kristo alipokuwa anakutana na mgonjwa, kabla  ya kumponya alikuwa  akimuuliza “Je, unaamini?”. Lengo la swali kama hili ni kutaka kufahamu, je mtu huyu anao utayari kwa kupokea uponyaji? Inabidi awepo mtu  aliye tayari kubadilika. Kwa Yesu 'hakuna kujaribu’ bali kuna kudhamiria kupokea sawa sawa na imani  yako kwake. Kama unataka kumiliki ujiandae kuua visivyotakiwa kuwepo. Kwenye  Baraka zako, yupo Goliath anayekuzuia. Daudi alipomuoana Goliath, alisema “huyu  ni nani anayetukana majeshi ya Mungu aliye hai? Wakati umewadia ambapo Lazima kizazi cha Daudi kiamke katika taifa letu kwa Jina la Yesu.  Huu siyo  wakati  tena wa kuongozwa  na viongozi wanaotumia nguvu za giza. Siyo wakati tena wa kuongozwa na viongozi wanaoenda kwa waganga wa kienyeji ili kupata nguvu au uongozi. Je, hayupo Mungu  katika taifa hili hata watu hawa wazitegemee nguvu za giza?

 

Wapo waliokuibia urithi wako wakakugawia mateso na magonjwa,  na leo hii ni wakati wako wa kupambana ili  kurudia kilicho chako. Mtu anayeomba na asiyeomba ni watu wawili tofauti. Anayeacha maombi, humpa nafasi shetani kukaa ndani ya moyo wake. Ndiyo maana migawo ya kishetani inaendelea kuwepo kwa sababu mtu  apewaye  huo mgawo hana nguvu ya kuikaataa.

 

Imeandikwa 2NYAKATI 32:8…[kwake upo mkono wa mwili; ila kwetu yupo Bwana, Mungu wetu, kutusaidia, na kutupigania mapigano yetu. Na watu wakayategemea maneno ya Hezekia, mfalme wa Yuda.]…. Mgawo wa kishetani una mkono wa mwili, mkono wa kibinadamu. Leo kataa kuwa chini ya mgawo wa kishetani  ambao adui amekugawia kwa Jina la Bwana. Upo  mkono wa Bwana kukusaidia ili kuangamiza kila  mgawo  wa kishetani maishani  mwako.  Kumbuka kuwa ndani mwako kuna mkono wa Bwana wa kukusaidia, kama Hezekiah alivyosema, kwa Jina la Yesu.

 

Kila "mgawo wa kishetani" utaweza tu kuuangamiza endapo umempokwa Yesu Kristo  maishani  mwako. Endapo mtu hujaokoka, chukua hatua ya kumpokea Yesu Kristo  maishani mwako, ili uweze kuiangamiza migawo yote ya kishetani  maishani mwako.

 

UKIRI
Kila  mgawo wa kishetani  uteketee kwa Jina la Yesu.  Leo naenda kinyume na kila mgawo wa kishetani maishani mwangu. Kila  uzao wa giza leo ninauteketeza kwa Jina la Yesu. Ninaikataa migawo yote ya mashetani. Leo ninakataa kupatana na wachawi. Achieni maisha yangu kwa Jina laYesu. Amen

 

 

=== © Information Ministry ===

(Ufufuo Na Uzima - Morogoro)

Mtaa wa Nguvu Kazi, (Minara Mitatu), Mkundi-Morogoro.

 /or

Contact our Church Leadreship:

 Bishop Dr. Godson Issa Zacharia

 (Glory of Christ (Tanzania) Church inMorogoro)

Cellphone: (+255) 765979866 /or +255 713459545

 
Share:

Monday, July 13, 2015

SOMO: NGUVU YA KIAPO-Na: BRYSON LEMA (RP)


JUMAPILI:  12 JULY 2015 - UFUFUO NA UZIMA MOROGORO

  

Utangulizi: Hivi kiapo ni kitu gani? Na kwa nini watu wanaapa? Kwa muhtasari, kama kiapo hakina mahusiano yoyote na Mungu au na wanadamu, hakuna ambaye angekifanya. Mungu naye huapa, na wanadamu vivyo hivyo. Imeandikwa katika EBRANIA 6:16-17…[Maana wanadamu huapa kwa yeye aliye mkuu kuliko wao; na kwao ukomo wa mashindano yote ya maneno ni kiapo, kwa kuyathibitisha. 17 Katika neno hilo Mungu, akitaka kuwaonyesha zaidi sana warithio ile ahadi, jinsi mashauri yake yasivyoweza kubadilika, alitia kiapo katikati;]….Maana yake,  mtu  aapo anaweka rehani uhai wake. Ni kuyaweka maisha yako  katika kile unachokiapia. Kumbuka kuwa uhai wa mwanadamu ndicho kitu cha thamani kuliko  vyote alivyo navyo. Ndiyo kusema kwamba, endapo  mwanadamu hana uhai ni sawa na ‘takataka’ tu. Tunasema hivyo kwa sababu ukeshachimbia shimo kitu na kukiweka huko, maana yake kile ulichokiweka huko ni takataka tu.

 

Kiapo ni njia ya mwisho kuliko zote aitumiayo mwanadamu kuondoa mabishano. Mtu umkutapo anaapa, huapa kwa jina la wazazi wake au jina la miungu  yake. Kwa nini iwe hivyo: ni kwa sababu wazazi ndio walio wakuu kuliko wote kwa maisha ya huyo mtu. Endapo mtu ataapa kwa jina la Mungu, nayo itategemea,  je huyu mtu ameapa kwa Mungu wa herufi ndogo (mungu, ambaye pia ni  shetani) au MUNGU wa Herufi  Kubwa (yaani Jehovah).

 

Katika ulimwengu wa roho kiapo ni kitu cha thmani sana. Unaposema ninaapa, maana yake unajiweka kwenye nafasi ya hicho kitu. Tunaona kuwa Mtu anapodhamiria kuapa anayaweka maisha yake rehani. Mtu afanyapo kiapo,  atahakikisha kuwa maisha yake  yule aliyemdhamiria katika hicho kiapo hayatakaa sawa hata kidogo.

 

Imeandikwa hivi katika MARKO 5:2-7 ..[ Na alipokwisha kushuka chomboni, mara alikutana na mtu, ambaye ametoka makaburini, mwenye pepo mchafu; 3 makao yake yalikuwa pale makaburini; wala hakuna mtu ye yote aliyeweza kumfunga tena, hata kwa minyororo; 4 kwa sababu alikuwa amefungwa mara nyingi kwa pingu na minyororo, akaikata ile minyororo, na kuzivunjavunja zile pingu; wala hakuna mtu aliyekuwa na nguvu za kumshinda. 5 Na sikuzote, usiku na mchana, alikuwako makaburini na milimani, akipiga kelele na kujikatakata kwa mawe. 6 Na alipomwona Yesu kwa mbali, alipiga mbio, akamsujudia; 7 akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese.]…. Ukisoma maandiko, Huyo ndiyo pepo pekee aliyehojiana na Yesu Kristo. Pia ndiye pepo pekee ambaye Yesu Kristo alimuuliza jina lake ni nani? Kilichomfanya atoe ruhusa ya hao pepo kuwaingia wale nguruwe ni kwa sababu alimwapisha Yesu Kristo kwa Mungu. Pepo hili lilijua ‘nguvu ya kiapo’. Washirikiana nao wanaijua hii nguvu ya kiapo, na ndiyo maana huifanya afya ya mtu isiwe nzuri, au maisha yake kwa sababu kuna  watu walioweka kiapo mahali  fulani. Kumbuka kuwa, kiapo kinapofanywa,  walinzi wa kiapo  nao huwekwa ili kusimamia hicho kiapo.

 

Kafara ya kiapo hutofautiana kulingana na ukubwa wa kile kilichotolewa.  Kafara ni kama sadaka ambayo hchinjwa (kuku,  kondooo,mbuzi, ng’ombe au ikizidi sana mwanadamu). Damu ya hizi kafara zikiwamwagika, huongea zikiwa ardhini. Ndiyo maana Biblia inasema ‘Damu ya Yesu hunena mema juu yetu’. Hata Pilato alipokuwa akimhukumu Yesu Kristo, alinawa mikono yake na kusema ‘Damu ya mtu huyu hainihusu’.  Leo hii tupo huru kutokana na kafara ya Kalvari ya Damu ya Yesu Krsito. Endapo hii Damu  ya Yesu hadi leo inanena mema juu yetu, je, hizi kafara za waganga wa kienyeji na wachawi wanazotoa kwa ajili  yako zinanena kitu gani?

 

Wakati mwingine maisha yetu hayaendi vizuri kwa sababu ya kukamatwa na viapo. JOSHUA 6:26…[Naye Yoshua akawaapisha kiapo wakati ule, akasema, Na alaaniwe mbele za Bwana mtu yule atakayeinuka na kuujenga tena mji huu wa Yeriko; ataweka msingi wake kwa kufiliwa na mzaliwa wa kwanza wake, tena atayasimamisha malango yake kwa kufiliwa na mtoto wake mwanamume aliye mdogo.]…. Joshua aliweka kiapo hiki kwa Jina la Bwana, Mungu aliye mkuu kuliko wote. Ni kitu gani  kilitokea kwa wale walioinuka kuujenga huu ukuta baada ya muda mrefu sana kupita tokea kuwekwa kwa hiki kiapo? Imeandikwa katika 1WAFALME 16:34 ….[Katika siku zake, Hieli Mbetheli akajenga Yeriko; akatia misingi yake kwa kufiwa na Abiramu mzaliwa wake wa kwanza   na kuyaweka malango yake kwa kufiwa na mwana wake mdogo Segubu; sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa Yoshua   mwana wa Nuni.]… Kile kiapo  kilikuwa hai, ingawa wale waliokuwepo wakati Joshua anaapisha wale watu walikuwa walishakufa. Kiapo chaweza kuwa hai, na kufuatilia maisha ya mtu wakati wowote ule. Katika familia zetu za Kiafrika, mambo mengi hayaendi kwa sababu vipo viapo  ambavyo mababu zetu walivifanya, na usipokuwa makini  kujitoa humo, utaendelea na aina hiyo  ya maisha magumu.

 

Zipo  koo ambazo mapatano yalifanyika zamani  sana bila wewe kujua. Inawezekana kweli hujawahi kwenda kwa waganga wa  kienyeji, lakini unajua je kama babu au bibi yako  hakuwahi  kwenda kwa hao waganga wa kienyeji? Pengine babu yako  aliweka mapatano hayo enzi hizo na waganga wa kienyeji,  na kwa sababu hiyo familia yako inaendelea kufuatiliwa. Chale zifanywazo na waganga wa kienyeji  ni mojawapo ya aina za viapo. Ni kwa sababu damu ni uhai (kwa mujibu wa Biblia). Kila damu ina vinasaba (DNA), na pale waganga wakizichanganya, hufanya watu wa aina hii kupitia maisha yasiyokuwa yao.

 

Katika familia zetu kuna uwezekano wa mmoja wapo kuunganisha hiyo familia na kuzimu. Katika wale 12 wanafanuzi  wa Yesu Kristo, mmojawao alikuwa ni  shetani. Watu  wanaweza kuweka mapatano  na kuzimu. Pengine afanyaye hayo yote atakuwa tayari kukusaidia kwa kila jambo, ili usimgundue. Miili  yetu hii ni sawa na  majumba tu. Kumbuka ukiwa na nyumba unaweza kuwa ndani ya hiyo nyumba au ukawa nje ya hiyo nyumba. Katika ulimwengu tuliopo sasa,  usiamini mwanadamu wa nje, ila muhimu ni ile roho ndani mwake, kwa sababu mtu ni roho na siyo  mwili.

 

Kipo kiapo ambacho mababu zangu au baba yangu alikifanya,  leo ni saa ya kuvivunja hivyo viapo vyao kwa Jina la Yesu. Sikuja hapa duniani hivi hivi, na hata mimi ninacho kiapo changu.  Imeandikwa katika 1WAFALME 2:43…[Mbona basi hukukishika kiapo cha Bwana, na amri niliyokuagiza?]… Kumbe basi kipo KIAPO CHA BWANA. Kama wao walienda kwa mizimu na kuapa, hata mimi ninao uwezo wa kuweka kiapo na Bwana, kwa sababu kiapo huondoa mabishano. Ni wakati wa kuondoa ubishani. Kiapo cha Bwana kitakomesha kila balaa ndani ya maisha yangu. Kumbuka kuwa, Mungu wetu anapoapa huapa kwa nafsi yake  mwenyewe. Siyo kama miungu ya dini zingine ambayo huapa kwa vitu vilivyoumbwa.

 

Uonapo dada yako ana matatizo yanayofanana na wewe, jiulize kwa nini  iwe hivyo wakati ninyi wawili mpo tofauti? Unapomuona kaka yako ana matatizo yanayofanana na wewe, jiulize kwa nini  iwe hivyo wakati ninyi wawili mpo tofauti? Haya yote yametokea kwa sababu kuna kiapo mahali fulani na wapo waliokaa kwenye hico kikao cha kiapo na kusababisha hayo uyaonayo yaendele kutokea. Ni  saa ya kukata kila  mnyororo wa kiapo kwenye familia yako. Ni saa ya kutoa kiapo na kuweka kiapo.

 

WAEBRANIA 7:20….[  Na kwa kuwa haikuwa pasipo kiapo,]…. Hakuna kitu kilichofanyika pasipo  kiapo. Na ndiyo maana ili Mungu atende jambo, aliapa. Maana yake, mambo yangu pia hayafanikiwi kwa sababu hakuna kiapo.  Endapo hakuna kiapo, maisha yako yanakuwa na matatizo. Ndiyo maana hata shetani alishindwa kumgusa Ayubu kwa sababu kati ya Mungu  na Ayubu palikuwepo na KIAPO. Cha wewe kufanya ni kuamua yafuatayo:-  Sina msamaha na mchawi anayeniwangia usiku. Biblia inasema, “usimwache mwanamke mchawi kuishi”.  Kumbuka  Mungu huyuhuyu  ni Yule aliyesema “usiue”,  lakini kwa habari  ya wachawi na washirikina Mungu ameruhusu wasiishi, maana yake wauawe.

 

Israeli waliongozwa usiku na mchana, bila hata adui mmoja kuwasogelea wakati wanaenda zao nchi ya Ahadi. Lile wingu lililowaongoza mchana, kwa sababu  ya kile  kiapo cha  Mungu  na Ibrahimu  kwamba uzao  wake atawapa hiyo nchi. Hata kwa sasa, kinachowafanya Israeli wakae salama ni kwa sababu ya kile kiapo walichokifanya, kwa kusema “Damu yake  (Yesu) iwe juu yetu na juu ya kizazi chetu”. Ingawa hawakujua wasemacho, hata sasa Damu ya Yesu inazidi kunena mema juu  yao. Daudi alikosea kwa kuwahesabu Israeli yote,  na adhabu ambayo Mungu alimpatia achague mojawapo ya hizi zilivyoandikwa katika 2SAMWELI 24:13-14 … [ Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza, akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma.14 Naye Daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu.]… Maana yake ni kuwa, nchi yote ya Israeli ilikuwa iadhibiwe kutokana na kosa la Daudi kama  kiongozi wao.  Endapo vipo “Viapo vya Kishetani” vilivyowekwa na viongozi wa serikali yetu leo lazima tuvivunje kwa Jina la Yesu. Viapo vya kishetani vilivyowekwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza, au Awamu ya Pili au Awamu ya Tatu au ya Nne lazima tuvivunje kwa Jina la Yesu.  

 

Je, umemwamini  Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wako? Huwezi kuweka kiapo na Mungu ambaye hujapatana naye. Unapoamua kuokoka unakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuvunja viapo vyote vivlvyowekwa kinyume nawe, na utaweza kuweka kiapo na Bwana Mungu, aliye Mungu Mkuu  kuliko miungu  yote, kwa Jina la Yesu.

 

UKIRI
Kuanzia sasa kila kiapo cha giza niachie, wote walioshika afya yangu, au maisha yangu  leo nawasambaratisha kwa Jina la Yesu. Viapo vyote vilivyofanyawa juu ya maisha yangu naviharibu  kwa Damu ya Mwanakondoo. Amen

 

 

=== © Information Ministry ===

(Ufufuo Na Uzima - Morogoro)

Mtaa wa Nguvu Kazi, (Minara Mitatu), Mkundi-Morogoro.

 /or

Contact our Church Leadreship:

 Bishop Dr. Godson Issa Zacharia

 (Glory of Christ (Tanzania) Church in Morogoro)

Cellphone: (+255) 765979866 /or +255 713459545

 
Share:

Monday, July 6, 2015

KUUSHINDA ULIMWENGU - Na: BRYSON LEMA (RP)


JUMAPILI:  05 JULY 2015 - UFUFUO NA UZIMA MOROGORO

 

Utangulizi: Wale wanaokuonea na kuyasumbua maisha yako  huitwa “watu wa ulimwengu huu”. Ukumbuke kuwa huu ulimwengu upo chini ya yule adui yetu shetani. GALATIA 1:4…[ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili ya dhambi zetu, ili atuokoe na dunia hii mbovu iliyopo sasa, kama alivyopenda Mungu, Baba yetu.]… Je, dunia ndiyo mbaya au wakaao duniani ndio wabaya? Je, Mungu aliumba kitu au vitu vibovu. Mungu ndiye aliiumba hii dunia. MWANZO 1:1-31, uumbaji wa Mungu unaonekana,  na kila alichokiumba  Mungu alisema ni kizuri, tena kinachopendeza.  Kwa kawaida kitu kizuri kinachopendeza hata siku moja siwezi kukiita kibovu. Mungu aliiacha dunia ikiwa inapendeza. Kipo kitu kilichotokea na kuifanya dunia iwe mbovu.

 

1YOHANA 1:4-5…[Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu. 5 Mwenye kuushinda ulimwengu ni nani, isipokuwa ni yeye aaminiye ya kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?]… Mtu aliyeushinda ulimwengu ni yule aliyemkiri Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yake.

 

Imeandikwa 1YOHANA 5:19…[Twajua ya kuwa sisi tu wa Mungu; na dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.]… Hapa tunagundua kuwa dunia hii inatawaliwa na shetani. Na mimi ambaye nimeokoka, sipo upande wa hii dunia. Kama dunia haipo upande wangu, ina maana  ya kwamba shetani anaweza kuwatumia wale wote wasiomwamini Yesu (ambao wapo duniani) ili kunipinga.  Ndiyo maana Yesu Kristo aliniokoa mimi na wewe kama mbegu ya kuzitikisa falme za hii dunia ili zote ziwe falme za mwanakondoo. Watu wa ulimwengu wanakupinga lakini Baba wa mbinguni alikujua na kukuandaa ili kuushinda ulimwengu na hiyo balaa iliyokuja mbele zako. Sikuzaliwa chini ya utumwa, bali nina kazi maalumu kwa ajili ya ushindi niliyopewa na Baba wa Mbinguni. Huyo adui anayekupinga hana kitu kwako, kwa sababu unayo mamlaka ya ushindi. Kabla ya vita yako, mshindi ameshatangazwa. Tatizo ni kuwa adui anayakamata mawazo na akili zako ili ujione kuwa uwezo wako ni huo kumbe siyo. Mamlaka na uwezo na nguvu ulizo nazo vyote ni vya Mungu, na kama Mungu hawezi na mimi siwezi. Ila kama Mungu anaweza na mimi naweza. Ndiyo maaana imeandikwa “waliozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu”. Yawezekana siyo leo au kesho lakini ninachokijua ni kuwa sitaondoka hapa kama aliyeshindwa bali kama mshindi.

 

Biblia inasema ujapopita katika bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa mabaya. Kwa kuangalia kwa macho unaona mauti, lakini mbele za Baba anona hayo mapito kama ‘uvuli wa mauti’.  Acha kulia na kusema maisha ni magumu. Kumbuka kuwa kati ya nuru na giza, chenye nguvu zaidi ya kingine ni nuru kwa sababu mahali penye giza ikiwekwa nuru giza hukimbia.  Kwa kuwa wewe umeokoka, ujue kuwa wewe ni nuru na wote walio gizani lazima wakimbie mbele zako. MATHAYO 5:13-16…[Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. 14 Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. 15 Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. 16 Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.]… Wanaokupinga wakikuangalia wanaona kitu kinang’aa na ndipo hutafuta namna ya kuifunika nuru yako. Wasichokijua ni kuwa hiyo nuru yako haijatoka kwa wanadamu. Giza haliwezi  kuiondoa nuru mahali popote. Fahamu kuwa waganga wa kienyeji ni giza. Ukiona giza linakufuatia ujue kuwa kuna mahali  ambapo taa yako imezimika. Inapaswa kuiwasha taa yako ili  kuifukuza giza mbele yako.

 

Kiu ya shetani ni kunizua nisitoke. Hata hivyo, sikuja kupata mafanikio kupitia watu ila mafanikio yangu yanatoka kwa Baba wa Mbinguni. Mtu unayemuona leo ni wa leo, ila usichokiona ni kesho yake mtu huyu.

 

Fahamu kuwa kazi ya shetani ni kukupinga na kukufunga. Imeandikwa  katika ISAYA 14:17…[Aliyeufanya ulimwengu ukiwa, akaipindua miji yake; Asiyewafungua wafungwa wake waende kwao? ]… Mpango wa shetani na mawakala wake ni kuwafunga watu wasiweze kwenda kwenye ushindi wao. Hupaswi kuwaza juu ya mamlaka aliyo nayo wakala wa shetani (adui). Mamlaka uliyo nayo ni makubwa kuliko ya adui zako. Haipaswi kukaa ndani ya kanisa ambalo watu wake wanamtegemea tu Mchungaji wao kuwaombea kila wakati. Unapaswa kukaa kanisani ambapo unapata maarifa ya kuomba mwenyewe,  kwa sababu  hata huyo mchungaji wako anakuwa na mambo yake binafsi ya kuombea, na hawezi kuanza kukuombea wewe kabla ya yale ya kwake.

 

Andiko mojawapo la kukutia nguvu lipo katika YOHANA 14:30…[Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.]…. Ina maana kwamba, huyo  mkuu wa ulimwengu hata kwako hana uwezo katika maisha yako. Kushindana watashindana nami, lakini hawatanishinda. Kuwepo katikati ya mapambano siyo tatizo, kwa sababu hata mimi ni mmojawapo wa wanaopigana. Vita vikiwa mbele yako havipo kwa ajili ya kukuangamiza,  bali kwa ajili ya  wewe kushinda.

 

Msogelee  adui wa maisha yako,  ndoa yako, biashara yako n.k. siyo kwa sababu nyingine bali ni kwa Jina la Bwana wa majeshi. Usihesabu matatizo uliyo nayo bali hesabu ushindi ulio nao ndani  ya  Kristo. Imeandikwa “mateso ya mwenye haki ni mengi lakini Bwana humponuya nayo yote”.

 

MHUBIRI 9:11…[Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati huwapata wote.]… Kuna wakati wa kila jambo ndani ya maisha yangu. Maisha yako  hayatakaa katika ugumu wakati wote.  Ndege akipita juu  ya kichwa changu siyo tatizo lakini tatizo ni huyo ndege kutengeneza kiota chake juu ya kichwa changu.  Ukiona mambo yanazidi kuwa magumu, jua kuwa ushindi nao unakaribia.

 

Wanaokupiga vita wanakusaidia kwenda kutawala. Yuda Iskariote kwa kumuuza Yesu Kristo alisababisha Yesu afe na baada ya siku ya tatu YESU akafufuka na kupewa JINA LIPITALO MAJINA YOTE. Siyo wakati wa kumlaumu Penina, kwa sababu bila Penina hakuna Samweli. Hanna alimimina maombi yake mbele za Bwana kwa sababu ya Penina kumchokoza. Eli  hakuwahi kumuona Hanna akiomboleza,  lakini baada ya kuinuka Penina ndiposa Eli akakutana na Hanna na kumwambia “Bwana na akupatie haja ya moyo wako”. Nipo kanisani kwa sababu ya Penina wa maisha yangu. Ni saa ya kukutana na Eli na kumwambia Eli shida ya maisha yako.

 

Je ,umempokea Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wa maisha yako? Kama upo na hujaokoka,  ni saa yako  kuanza upya kwa kuzaliwa upya .

 

=== © Information Ministry ===

(Ufufuo Na Uzima - Morogoro)

Mtaa wa Nguvu Kazi, (Minara Mitatu), Mkundi-Morogoro.

 /or

Contact our Church Leadreship:

 Bishop Dr. Godson Issa Zacharia

 (Glory of Christ (Tanzania) Church inMorogoro)

Cellphone: (+255) 765979866 /or +255 713459545

 

Share:
Powered by Blogger.

Pages