Sunday, February 25, 2018

BOMOA KUTA ZA KICHAWI ZILIZOKUZINGIRA

GLORY OF CHRIST TANZANIA CHURCH (GCTC)
KANISA LA UFUFUO NA UZIMA MOROGORO
PASTOR DR. GODSON ISSA ZACHARIA
JUMAPILI: 25 FEBRUARI, 2018
Mchungaji Kiongozi Dr. Godson Issa Zacharia akifundisha neno la Mungu kuhusu kubomoa kuta za Kichawi.

Kazi ya Ukuta au Boma ni kuzingira eneo la kitu fulana kwa namna ya ulinzi. Ukuta unajengwa kama kizuizi cha kuruhusu ni kitu gani/nani aingi na kutoka upande mmoja kwenda upande mwingine. Ukuta unavyoonekana katika majumba yetu kwa macho ya mwili ni sawa na kuta zinazojengwa katika maisha yetu katika ulimwengu usioonekana(wa roho).
“Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote;” Luka 19:43
Ukuta/Boma unaweza kujengwa na wachawi/waganga wa kienyeji ukakuzingira na kukuhusuru usifanikiwe. Miji yote unayoiona hapa dunia ina ukuta katika ulimwengu wa roho. Kuta hizi ndizo zinazomruhusu mtu gani asome nani asisome, nani apite nani asipite, na afe nani na nani asife. Kuta hizi zinachagua vitu gani vipite na vipi visipite. Lakini ukuta uliojengewa wewe ni ukuta ili usiweze kupita kwenda kwenye mafanikio yako lakini majini, mapepo, mashetani yanapita. Ukuta unakuhusuru, kuhusuru ni kifungo ambacho huwezi kutoka hata ndani ya ukuta hupigi hatua pia. Mfano wana wa Israeli walikuwa Samaria walipo husuriwa walikula mavi ya njiwa mpaka wakafikia hatua ya kula watoto wao wenyewe.
Huu ni ukuta maalum unakuzunguka ili usipatikane msaada kutoka nje. Watu wanakuja na fedha, dhahabu, mitaji lakini umezingirwa usipate msaada. Yamkini Mungu aliaanda watu waje wakusaidie ila mpaka leo hawajaja kwa sababu ya ukuta huo.
Wanaojenga ukuta wanaweka walinzi wa kichawi, kipepo. Ukuta huo pia una milango na milango hiyo ina walinzi. Walinzi wanawekwa kwa sababu unaweza ukaruka ukuta, kama ilivyoandikwa katika Biblia.
“Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi, Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.” Zaburi 18:29
Ikitokea umeruka ukuta walinzi hao wakukabili wakuvunje, wakupige hata mauti. Shetani anajua maandiko na ndio maana anaweka walinzi kwa sababu anajua unao uwezo wa kuruka. Walinzi wanawekwa kwa tahaadhari endapo utaruka ukuta.
“Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi; Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.” 2 Samweli 22:30
Baadhi ya Wana wa Ufufuo na Uzima wakifuatilia kwa makini wakati wa mafundisho ya neno la Mungu ili baadae waweze kuzibomoa kuta zilizozingira maisha yao.

Mfano watu wanapojenga nyumba wanaweka ukuta, na juu ya ukuta senyenge yenye umeme na bado wanaweka walinzi na mbwa pamoja na kamera na yote haya ni kwa ajili ya ulinzi. Na katika ulimwemgu wa roho shetani anafanya zaidi ya haya.
Kuna majeshi ya kuzimu, majeshi ya mauti, yamekulinda yanakufuatilia ili kukuangamiza bali wewe simama katika Kristo ili kukabili hayo majeshi. Maana maandiko yana sema kwa msaada wako nitalifuatilia jeshi.
Mfano mwingine Ulaya wamejenga ukuta ili kuwazuia Afrika Mangaribi ili wasiweze kuingia ulaya. Lakini wapo wanaojaribu kwenda wanapokuta na ukuta wanakamatwa na kurudishwa tena. Wanaenda Ulaya wakifikiria maisha mazuri yanapatikana huko tu, lakini huu ni ukuta wa akili kwa sababu bara la Afrika lina kila kitu.
Wanapoweka ukuta malengo yao ni ili usiruke, endepo utaruka ukuta walinzi waweze kukudhibiti. Na ukifanikiwa kuruka walinzi wanahojiwa imekuwaje mtu huyu karuka ukuta na hakutakiwa kuoa lakini ametangaza uchumba. Lakini leo ugeuke uwe mwali wa moto na uruke ukuta kwa jina la Yesu.
“Ee Bwana, uwakumbuke wana wa Edomu, Siku ya Yerusalemu. Waliosema, Bomoeni! Bomoeni hata misingini!” Zaburi 137:7
“Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa.” Matendo ya Mitume 16:26
Mchungaji Kiongozi akiomba ili kuzibomoa Kuta za Kichawi zilizozingira watu wa Morogoro na viunga vyake.

Tunajifunza Paulo na Sila walipokamatwa na kuwekwa gerezani, waliwekewa na walinzi. Misingi ikitikisika vifungo vinalegezwa, milango iliyofungwa inalegea kwa jina la Yesu. Milango ya laana, milango ya utasa, naifunga kwa jina la Yesu, nafungua milango ya mafanikio, milango ya kazi, ya biashara ipokee kwa jina la Yesu. Milango imefunguliwa na Bwana, asitokee hata mmoja wa kuifunga milango hiyo kwa jina la Yesu.
“Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.” Mathayo 18:18
Ukuta ni hatari, hata katika ulimwengu wa mwili ni hatari kwa sababu unatenga kati ya upande huu na upande ule. Yesu anajua athari za kujengewa ukuta au kuzingirwa pande zote. Yesu alipokuwa anaelekea Yerusalem alio ukuta watu wamejengewa, na Yesu alilia mji.
“Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, akisema, Laiti ungalijua, hata wewe katika siku hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua majira ya kujiliwa kwako.” Luka 19:41 - 44
Showers of Glory wakimsifu Mungu wakati wa Ibada ya leo.

Laiti ungelijua nguvu iliyo ndani yako, usingelala upige majeshi maana wachawi hawalali wanakesha wakikujengea ukuta. Inawezekana umefichwa na kisomo, fedha ulizonazo, umefichwa na uzuri ulio nao lakini kuna siku zinakuja adui zako watakujengea boma/ukuta na litakuzunguka na kukuhusuru wewe na watoto wako na kukupiga chini. Unatakiwa uamke kwenye huo usingizi ubomoe boma hilo kwa jina la Yesu. Wanapokujengea na kuangushwa chini ili usisimame tena, ukianza biashara ife, masomo yafe, lakini Bwana ana habari njema maana wao watainama na kuanguka ili wewe usimame na kuinuka. Shida ya kuzungukwa na boma ni kwa sababu hujajua majira yako. Hizi ni nyakati ambazo shetani anavaa mwili wa binadamu. Huu ni wakati ambao binadamu wanawakata wenzao kwa mapanga. Majira haya ni majira ya kufufua.
Ukizungushiwa ukuta kinachofuata ni uharibifu, kama kazi inakufa, ndoa inakufa. Samaria ilikuwa na fedha sana ndio sababu ya wale wakoma walitolewa nje ya mji. Akiba ya chakula na kila kitu kilikishwa, Jeshi la washami likauja ili kupigana nao. Ukizingirwa na ukuta wa kichawi walinzi ndio wanasababisha matatizo katika maisha yako.
“Lakini, hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia.” Luka 21:20
Yamkni umezingirwa kwenye kazi, masomoni, nyumba yako imekuwa tabu, lakini Bwana ana habari njema kwako ingawa tunaenda katika mwili hatufanyi vita juu ya mwili, wachawi, wasoma nyota mliotuzingira umefurahi sana ili nianguke lakini Bwana ananisimamisha tena. Waliokuhusuru leo wakazungukwe wao kwa jina la Yesu.
Baadhi ya Makutano ambao waliamua kumpa Yesu maisha yao ili awe Bwana na Mwokozi wa maisha yao.

Tunaona duniani kuna majeshi ya aina tatu, majeshi ya angani , majini na ardhini. Na katika ulimwengu wa roho wanamajeshi ya aina tatu pia. Unaporajibu kuruka ukuta unakutana na mapepo ya angani. Na walinzi wapo wa aina 3 wa ardhini, angani na majini. Unakuta mtu anakuja kukuletea masaada hawezi kwa sababu ya walinzi.
“Naye alipofika ng'ambo, katika nchi ya Wagerasi, watu wawili wenye pepo walikutana naye, wanatoka makaburini, wakali mno, hata mtu asiweze kuipitia njia ile.” Mathayo 8:28
Kwenye mlango kuna walinzi wakali mno ili usiingie katika Baraka zako. Kuna mtu anatakiwa akusaidie lakini kuna walinzi wakali mno wanamzuia asije. Njia ifanyike katika maisha yako kwa jina la Yesu. Walinzi wanaweza kulinda mji kama Morogoro, wakalinda ndoa yako, kazi, afya leo tunawafukuza kwa jina la Yesu.
Walinzi wanalinda mno, wapo tayari kuua ili msaada usikufikie. Kuna baadhi ya watu kila msaada unaotokea mara inashindikana. Walinzi hawa wanalinda hadi juu ya ukuta mtu asirukie Baraka zake.
Ukuta huu ulitengenezwa kwa ajili ya wana wa Israeli, kama ukuta uliweza kujengwa kwa wana wa Israel. Yeriko ilifungwa asipatikane aingiaye au atokaye. Inawezekana umejengewa ukuta ndo maana hakuna msaada kwa ndugu au marafiki. Lakini Bwana alimwambia Yoshua ameuweka mikononi mwako mji wa Yeriko.
“Basi Yeriko ulikuwa umefungwa kabisa kwa sababu ya wana wa Israeli; hapana mtu aliyetoka wala hapana mtu aliyeingia.” Yoshua 6:1

Yesu alipokufa aliwekewa walinzi na wakaambiwa walinde kadri wawezavyo. Walimlinda Yesu ili asifufuke. Na wewe unalindwa ili usitoke kuelekea kwenye mafanikio yako. Na siku ya tatu malaika alishuka kutoka mbingunii, walinzi wakawa kama marehemu. Walinzi waliokulinda kwenye taabu, shida leo waanguke wafe kwa jina la Yesu.
Ukuta ulijengwa Yericko kwa sababu zifuatazo:
Walisikia uvumi ya kwamba Mungu wao anawasaidia sana. Bahari ya shamu iligawanyika. Walipopata njaa Mungu alinyesha mvua ya mkate. Walipokosa nyama Mungu alinyesha mvua ya kware. Uvumi mwingine walipokosa maji walipiga mwamba na mwamba ukatoa maji. Uvumi mwingine walisafiri kwa mwendo wa miaka 40 jangwa lakini nguo zao ziko vizuri.
Kama kuna ukuta umejengwa kwenye maisha yako kwa sababu ya uvumi, leo lazima udondoke kwa jina la Yesu.
KWA MSAADA ZAIDI NA MAOMBEZI WASILIANA NASI KUPITIA
FACEBOOK: Pastor Dr Godson Issa Zacharia
Follow us on INSTAGRAM: pastordrgodson
Follow us on YOUTUBE: Pastor Dr.Godson Zacharia
TEL: +255 719 798778
BLOG: Ufufuo na Uzima Morogorohttp://ufufuonauzimamorogoro.blogspot.co m/
Share:
Powered by Blogger.

Pages